Tatizo la UsafirI wa Daladala Zanzibar

Kwa mkazi yeyote wa Zanzibar anayajua masaibu na shida zinazowakuta wasafiri wa ndani hasa wa masafa mafupi watumiao usafiri wa Ummah unaoitwa daladala.
Masaibu hayo yameonekana kushtadi kila uchao, huku mamlaka husika zikionekana kutochukua hatua thabiti kukabiliana na wimbi hilo.

Miongoni mwa masaibu hayo ni ukosefu wa vituo thabiti vya wasafiri (stands) vyenye huduma za msingi, kuanzia eneo la kutosha kwa wasafiri wanaokuja na kuondoka, huduma za choo, na zaidi eneo la kujistiri kwa kujihifahi na jua au mvua.

Pia wasafiri hukabiliana na msongamano mkubwa wa wasafiri, na hili ni imma kutokana na gari kuwa haba, na watu kuwa wengi, au uwepo gari nyingi, ila ndogondogo zisizoweza kubeba abiria wengi.

Karibuni Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Idara ya Usafiri na Leseni imekiri kuwepo kwa tatizo la ugumu wa usafiri wa daladala katika maeneo mengi ya Zanzibar, kupitia Mkurugenzi wa Idara ya Usafiri na Leseni ndugu Suleiman Kinoo Kirobo, hata hivyo, kama serikali baada ya kukabiliana na changamoto hizo amedai chanzo ni utaratibu mbaya wa utendaji kazi wa madereva wa huduma hiyo.
http://zanzibar24.co.tz/video-mamia-ya-abiria-wasota-vituo…/
Kwa ufupi badala ya serikali kuingilia na kutatua kero, inaungana na raia katika kusononeka.

Mbali na mashaka tuliyotaja pia wasafiri wa daladala husibiwa na ukatishaji wa safari kwa daladala nyingi kutokufia katika kituo kilichopangiwa, jambo ambalo huongeza gharama za usafiri, kwani humlazimu abiria apande gari zaidi ya moja, na kumfanya abiria agharamike kwa nauli ziada. Kama hilo haitoshi, wasafiri wa njiani wakati mwengine huwa kwao vigumu kupata usafiri, kwani mara nyingine wenye daladala wamekuwa wakiwaacha kwa kuchukua abiria wa mwisho wagari tu.

Pia wasafiri hao wamejikuta wakikosa usalama wa mali zao, wakilia uwepo wa vitendo vya kuibiwa mali zao mbalimbali katika msongamano wakiwa wameshughulika kugombania usafiri, kuna wahalifu hutumia muda huo kuwachomoa pesa, simu na vitu vyengine vya thamani.

Miundo mbinu pia changamoto, iko baadhi mibovu na, pia ile inayofanyiwa matengenezo, kama barabara ya Fuoni – Kwerekwe, Bubu- Mkokotoni nk. hilo nalo limechangia kudorora uharaka wa huduma ya usafiri huo wa Umma. Lakini pia baadhi ya wamiliki magari kuhamisha magari yao kutoka katika barabara hizo. Hilo limechangia tatizo kuwa kubwa, kwa kuleta foleni ambazo huchelewesha gari kwenda na kurudi kwa uharaka.

Aidha, kumekuwa na tatizo la wenye daladala kukosa morali wa kazi yao kutokana na malalamiko kuwa nauli haikidhi, kwani nauli ya sasa imetuama kwa muda mrefu bila ya kupanda, ilhali bei ya nishati ya mafuta inapanda. Hivyo, baadhi ya wamiliki wametoa magari yao katika huduma ya dala dala na kuyafanya ya usafiri wa kibinafsi kwa madai ya kukosa faida

Makundi yanayoteseka zaidi katika madhila na janga hili ni wanafunzi hususan wadogo wazee, wajawazito, wagonjwa, wazazi na wanawake wachamungu wanaochelea kupigana vikumbo na wanaume.

Tatizo hili ni kubwa katika ulimwengu wa sasa kwa miji mbalimbali hususan nchi changa, na serikali za nchi hizo hukosa ghera ya kukabiliana nalo ipasavyo.

Licha ya kuwa Uislamu hautoingilia katika kupanga bei katika biashara binafsi kama hizi daladala, lakini utasimamia kwa kuweka utaratibu mzuri na usalama wa raia kuanzia hali ya vyombo vya usafiri, mazingira ya vituo, wakati wa safari nk. Yaani kudhamini usalama wa wasafiri wote wawe Waislamu au wengine kuanzia mwanzo wa safari hadi mwisho.

سِيرُوا فِيهَا لَيَالِيَ وَأَيَّامًا آمِنِينَ (سبأ: 18

“Nendeni (safirini) humo usiku na mchana kwa amani” (TMQ 34:18)

Kwa mfano, dola ya Khilafah katika kupanga utaratibu mzuri itaweka kanuni ya kuwa na mabasi makubwa ya eneo la mijini ambayo yatabeba watu wengi zaidi. Hili litafanyika kwa kuwataka wafanyabiashara kununua mabasi makubwa, na kwa wale ambao hawana uwezo serikali itawawezesha kwa mikopo isiyo na riba kuhakikisha usahali wa wasafiri. Amma kuhusu usafiri wa wanafunzi, wagojwa na wasiojiweza hata kama wana nguvu zao bado ni jukumu la serikali kuhakkisha wanapata mahitaji yao ya usafiri na mengineyo kwa mujibu wa sheria.

Kwa upande wa miundo mbinu chini ya dola ya Kiislamu ya Khilafah itaimarishwa. Kwa kuwa jambo hilo ni miongoni mwa dhima ya mtawala wa Kiislamu. Ni wazi masuala kuanzia barabara nzuri, madaraja, vituo nk. yatashughulikiwa kadiri iwezekanavyo.

Imepokewa kwamba Khalifa Omar bin Khatwaab aliwahi kutamka kuwa ana khofu mbele ya Muumba wake kwenda kuulizwa kama mtoto wa ngamia atajikwaa njiani kwa kutoondosha adha njiani hapo. Hivyo, jukumu la kuweka miundo mbinu thabiti ni kiongozi na utawala wa Khilafah, na lau atashindwa na kupuuza kutenda hilo, hulazimu ahesabiwe na kuwajibishwa na Ummah.

Aidha, Uislamu unashurutisha Waislamu kuchunga mikataba yao, na jambo hilo hautoliachia kuwa la kibinafsi tu, bali dola utalisimamia vilivyo. Kutakuwa na makadhi muhtasib watakaosimamia haki za raia zisivunjwe, na kuchukua hatua hapo hapo. Hivyo kutahakikishwa mkataba wa gari wa kutoa huduma kutoka sehemu moja hadi nyengine unatimilizwa, na atakaevunja mkataba huo, sheria ya Allah sw inaanguka juu yake kuanzia hapa duniani.

Mbali na kuruhusiwa watu na makampuni binafsi kujihusisha na biashara ya kutoa huduma za usafiri kwa Ummah, pia dola ya Khilafah ikiwa kama ndio msimamizi wa mambo ya raia itakapoona kuna haja ya kujihusisha na huduma hiyo ili kuwarahisishia raia, italazimika kufanya hivyo.

Huo ndio usimamizi wa Khilafah kwa suala la usafiri na maisha kwa ujumla. Basi kwa Waislamu muitikieni Mola wenu (sw) na Mtume wake saw, kwani wao wanakuiteni katika mambo ya kheri ya dunia na akhera yenu. Na kwa wasiokuwa Waislamu, chukueni fursa kuutafiti kwa nia safi mfumo wa Kiislamu na utawala wake wa Khilafah.

20 Jumada al-Thanni 1440 Hijri | 25-02- 2019 Miladi

Afisi ya Habari – Hizb ut- Tahrir Tanzania

https://hizb.or.tz/
https://www.facebook.com/Hizb-ut-Tahrir-Tanzania

Maoni hayajaruhusiwa.