Mfumo Wa Ubepari Unajali Matajiri Na Si Wamachinga

بسم الله الرحمن الرحيم

Habari:
Mnamo tarehe 1/11/2021 Serikali ya Tanzania ilianza zoezi la kuwahamisha maeneo mengine wafanyabiashara ndogondogo nchini maarufu kama” wamachinga” kufuatia maagizo ya Raisi kwa wakuu wa mikoa na wasaidizi wao.
Maoni:
Suala kuhamishwa kwa wamachinga kwenda katika maeneo waliyotengewa siyo geni, kumekuwa na kampeni za aina hiyo katika miaka ya nyuma, kwa mfano ile ya mwaka 2016 iliyowapelekea kuhamishiwa maeneo mapya ya biashara kama vile Kigogo Fresh, Kivule, Ukonga na Tabata Muslim ambayo yalikuwa na uwezo wa kuchukua hadi wamachinga 6,000 lakini zoezi hilo haikufanikiwa.
Mara nyingi kwa kisingizio cha oparesheni kama hizi, Polisi kwa kushirikiana na askari mgambo wa Jiji hujihusisha kukamata,kubomoa vibanda vya na hata kupora kwa kufilisi bidhaa za wamachinga. Vitendo hivi visivyo vya kibinadamu vitaathiri wamachinga ambao ni takribani milioni nne nchi nzima kwa mujibu wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu, ambapo kati yao 50,000 wanapatikana katika jiji kuu la biashara Dar es Salaam (The East African 15/12/2018)
Ni ukweli usiopingika kuwa suala la wamachinga linahitaji suluhisho bora ili kuepusha matatizo na malalamiko mengi katika miji mikubwa ikiwemo kutozuiya njia za watembea kwa miguu nk. Hata hivyo, haya yanahitaji suluhisho lenye dhamira na utashi madhubuti na si maigizo ya kisiasa.
Wamachinga ni watu masikini wenye mitaji midogo sana wanaojaribu kujiajiri katika mfumo wa biashara usio rasmi, baada ya kushindwa kwa serikali kutoa ajira kwao. Kwa miaka takribani mitano iliyopita serikali haijaweza kutoa ajira inavyostahiki, hivyo watu wengi wakiwemo waliomaliza vyuo vikuu hawana ajira.
Ni wazi katika kukabiliana na suala hili, serikali kama zilivyo serikali nyingine za kibepari imeonesha kutowajibika, kiburi na kutojali raia kwani ina wajibu wa kuandaa mazingira bora kwa wamachinga kama inavyofanya kwa makampuni ya kibepari ya kimagharibi ambayo huja kunyonya rasilimali zetu kwa jina la uwekezaji wa kigeni.
Serikali inapaswa kuwasaidia wamachinga kwa kuwapatia maeneo muwafaka na rafiki kibiashara ili wafanye biashara kwa usahali hasa kwa kuzingatia kuwa serikali inakadiriwa kuwa ilikusanya takribani Tsh bilioni 80 (dolari milioni 34.7) kama ushuru kutoka kwa wamachinga kutokana na kuwauzia vitambulisho vya ujasiriamali ambavyo vilikuwa vinatolewa kwa wafanyabiashara ndogondogo wenye mitaji isiyozidi Tsh milioni 4 (dolari 1,900). Ajabu ! mara baada ya kukusanya pesa hizo sasa serikali inawageuka na kuwanyanyasa wamachinga hao!
Katika Uislamu, tofauti na Ubepari, jukumu msingi la serikali ya Kiislamu ya Khilafah ni kuwatumikia watu wote, kwani hiyo ni dhima na amana kubwa mbele ya Allah Taala. Khalifah-kiongozi wa serikali ya kiulimwengu ya Kiislamu, atabeba majukumu na dhima ya kuwatumikia raia wote bila ubaguzi. uwe wa kipato, dini, au rangi zao, dini zao, nk.
Imeandikwa na Said Bitomwa
Mwanachama wa Afisi ya Habari ya Hizb ut Tahrir Tanzania
Kwa ajili ya Afisi Kuu ya Habari ya Hizb ut Tahrir

Maoni hayajaruhusiwa.