Serikali na Viongozi wa Kisekula Hawana Huruma: Ukame Unaua Watu, Serikali na Viongozi Wanadai ni Taarifa “Feki”!

Wakenya takribani milioni 1.2 wamo hatarini kufa njaa kutokana na ukame. Na jumla zaidi ya Wakenya takribani milioni 14.7 hawana chakula kwa msimu huu wa kiangazi unaoendelea. Mamlaka ya Kitaifa ya Kusimamia Kiangazi (NDMA) ilitaja hali hii imetokamana na ukosefu wa mvua, mkurupuko wa maradhi, uvamizi wa nzige na ukosefu wa usalama. Kwa upande wake, Serikali imekana madai ya kuwa watu kadhaa wamekufa njaa. Kwani Mamlaka ya Kitaifa ya Kusimamia Majanga kupitia Mtendaji Mkuu James Oduor, ilisema kuwa vyombo vya habari vimezikuza ripoti za kufariki na kupelekea taarifa za makosa kwa ummah. Na kuongeza kusema kuwa “Ni kweli vifo vimetokea lakini haviwezi kuhusishwa moja kwa moja na kiangazi. Inawezekana kuwa ni kutokana na ugonjwa na masuala mengine.” (The Star, 18/03/2019).

Ili kujua chimbuko la janga hili ni muhimu Wakenya wenye akili timamu kufahamu kuwa Kenya ina bebeshwa itikadi ya Kisekula (Kutenganisha dini na maisha) na mfumo wake batili wa Urasilimali (Kipaombele ni maslahi/manufaa), hivyo inaendesha utawala wake kwa mujibu wa mfumo huu muovu. Kwa kufahamu hayo ndio utajua kuwa tatizo hilo limesababishwa na Serikali za kisekula ikiwemo Kenya:

Kwanza, Hazithamini raia wake hii ni kwa kuwa huwaangalia raia kama watumwa katika majumba na viwanda/makampuni yao na kisha kuwalipa vijifedha vya kununulia chakula ili wasife na waendelee kuwatumikia daima. Akiba ndogo walizo nazo zinaporwa kwa njia ya ushuru kwa mwito wa kisanii eti “kulipa ushuru ni kujitegemea.” Jukumu lao kubwa baada ya utumwa na ulipaji ushuru ni kuhalalisha utawala na viongozi vibaraka wakoloni kuingia au kubakia mamlakani kwa kupiga kura daima ambazo huwapa mamlaka utawala na viongozi wake kutunga sheria kinyume na za Muumba na kuendelea kuwakandamiza kupitia sera fisidifu za kirasilimali ikiwemo uchumi uliomakinishwa juu ya mikopo ya riba na utozwaji ushuru daima!

Pili, Hukuza suala la uhaba/uchache wa bidhaa na huduma ili kumakinisha tatizo la kiuchumi la kirongo ili kuendelea kuwakandamiza raia jumla. Ukweli ni kwamba tatizo la kiuchumi ni usambazaji wa mali kwa ukamilifu. Mfano hivi sasa watu wanafariki kwa ukosefu wa chakula lakini miezi ya nyuma tulishuhudia mamia ya magari yaliyojaa mahindi yakiharibika wenyewe wasijue pakuyapeleka, miaka ya nyuma tulishuhudia kiwanda cha Kitaifa cha Maziwa kikimwaga maziwa mengi eti kwa kuwa hawana mahali paziada pakuweka maziwa ziada na hivi majuzi maghala ya kitaifa yalipoteza magunia takribani 750,000 ya thamani ya bilioni Sh1.8 kwa kuwekwa vibaya! Yote haya ni kwa ajili ya kuendeleza urongo wa tatizo la kiuchumi wa kirasilimali!

Tatu, Kupata shida na kupelekea kufa kwa raia ni moja katika mbinu za kupunguza watu kama zilivyo mbinu za kupanga uzazi ili kuweza kutatua eti tatizo la watu wengi ikilinganishwa na uhaba wa bidhaa na huduma kwa mujibu wa mtizamo wa sera ya uchumi wa kirasilimali! Ndio maana serikali haioni wasiwasi watu wakifa! Thamani ya raia ni mchango wao katika ukuaji wa uchumi wa taifa na hivyo basi ikiwa hawana mchango wowote basi ni bora afilie mbali na huku wakidai ni taarifa feki!

Nne, Julai, 2011 Wakenya walifyonzwa takribani bilioni Sh1 kupitia Kampeni iliyoendeshwa na makampuni makubwa kwa ushirikiano na Red Cross eti kuchangisha pesa ili kuweza kupambana na ukame katika Kaunti ya Turkana! La kusikitisha ni kuwa mwaka mmoja kabla (2010) Kenya ilitumia mabilioni ya pesa eti Kupitisha Katiba Mpya ambapo tuliwashuhudia viongozi vibaraka wakienda huku na kule wakiipigia debe lakini kulipozuka tatizo la kujirudiarudia la UKAME hawakuonenaka isipokuwa wachache waliotaka kulidandia suala hilo kisiasa!

Suluhisho msingi kwa Kenya na Afrika kwa ujumla ni kukumbatia ulinganizi wa kurudisha tena maisha ya Kiislamu kwa kusimamisha Serikali ya Kiislamu ya Khilafah kwa njia ya Utume. Khilafah itakayosimama juu ya msingi wa Shari’ah (Qur’an na Sunnah) inayotoka kwa Mwenyezi Mungu (swt). Khilafah itakuwepo kuwapa utulivu, maendeleo na ustawi raia wake Waislamu na wasiokuwa Waislamu. Khilafah haitopiga hesabu zake kwa misingi ya maslahi/manufaa kama ilivyo leo chini ya serikali za kisekula ambazo zinakwenda mbio kuhakikisha Pato la Taifa linakuwa na huku umasikini unaendelea kukuwa miongoni mwa watu na pengo kati ya matajiri na masikini likizidi kwa kasi mno! Khilafah itasimamiwa na kiongozi Khalifah mchajimungu sio kibaraka ambaye kibla chake ni Washington, London au Paris n.k. Khalifah atakayekwenda mbio akijua kuwa Siku ya Kiyama atakwenda kuulizwa na Mwenyezi Mungu (swt) kuhusu usimamizi wake juu ya watu anaowasimamia. Mtume (saw) alisema:

«الإِمَامُ رَاعٍ وَمَسْؤولٌ عَنْ رَعِيَّتِهِ»

“Imamu (Khalifah) ni msimamizi /mchungaji na ataulizwa juu ya anaowachunga”

Khalifah atakayekuwa hali isipokuwa mpaka baada ya raia wake wameshiba na akihakikisha kuwa usambazaji wa mali/chakula kwa raia wake ndani ya Khilafah unafanyika kwa njia bora kama ilivyokuwa wakati wa Khalifah Umar ibn al-Khattab (ra) “ aliyegawa chakula mwenyewe kwa raia wake baada ya kuwa Madinatul Munawarrah imekumbwa na ukame na yeye mwenyewe akilala njaa licha ya kuwa ni Khalifah kiongozi wa Dola kubwa duniani!” Si hivyo tu bali alikuwa akitembea ndani ya mji ili kujua ikiwa raia wake wako salama na kwamba mahitaji yao yamekidhiwa. Na siku moja usiku alipokuwa katika ziara zake “akapita pembezoni mwa nyumba iliyokuwa ina mwangaza na kusikia sauti za watoto wakilia. Baada ya kubisha na kupewa ruhusa kuingia ndani akamuona mwanamke yuko jikoni na kando yake kuna watoto wanalia. Akamuuliza kuhusu watoto, mumewe na alichokuwa anapika akasema ni watoto wake na mumewe alifariki na kwamba mule ndani ya sufuria mulikuwa na mawe na maji alikuwa anafanya kama ambaye anakoroga ili watoto wawe na matumaini ya chakula kisha wapatilizwe na usingizi ategue sufuria hiyo! Na mwanamke huyo akaongeza kusema kuwa “Namlaumu Khalifah wetu Umar kwa hali hii ngumu tunayopitia. Khalifaf Umar ibn al-Khattab (ra) akashtuka mno na kukimbilia katika Baitul Mal na kuchukua chakula na kukibeba mabegani mwake na kumpelekea mwanamke yule na kumsaidia katika kupika mpaka akaivisha na watoto kula na kabla aondoke akaahidi kuwa kuanzia wakati ule mahitaji yao yataendelea kuletwa!

Hivyo ndivyo hali za raia zilivyokuwa na zitakavyokuwa chini ya Khilafah inayoongozwa na kiongozi Khalifah mchamungu. Kinyume na leo hii viongozi vibaraka masekula wasiokuwa na huruma na wako tayari kukulipia gharama yako ya mazishi lakini hawako tayari kusimamia mahitaji yako msingi au hata kukupa chakula wakati wa ukame! Ilhali majumbani mwao mbwa wao wanakula nyama na pizza! Tunapoendelea kuwa mbali na Maamrisho ya Mwenyezi Mungu naye ataendele kutupa shida:

(وَمَنْ أَعْرَضَ عَن ذِكْرِي فَإِنَّ لَهُ مَعِيشَةً ضَنكاً وَنَحْشُرُهُ يَوْمَ الْقِيَامَةِ أَعْمَىٰ)

“Na atakaye jiepusha na mawaidha yangu, basi kwa yakini atapata maisha yenye dhiki, na Siku ya Kiyama tutamfufua hali ya kuwa ni kipofu” [Ta-Ha: 124]

Ali Nassoro Ali

Mwanachama wa Afisi ya Habari ya Hizb ut Tahrir Kenya

Makala Na.37: Ijumaa, 15 Rajab 1440 | 2019/03/22

Inatoka:  http://hizb.or.ke/sw/2019/03/22/serikali-na-viongozi-wa-kisekula-hawana-huruma-ukame-unaua-watu-serikali-na-viongozi-wanadai-ni-taarifa-feki/

Maoni hayajaruhusiwa.