Marekani Ilivyotumia Tukio La Septemba 11 Kuupiga Vita Uislamu

بسم الله الرحمن الرحيم

Wiki iliyopita ndani ya tarehe 11 Septemba, ndio siku ambayo taifa la Marekani hufanya kumbukumbu ya tukio linaloitwa la kigaidi lililotokea nchini humo tarehe kama hiyo mwaka 2001.
Tukio hilo lenye utata lilitokea baada ya kile kilichoelezwa na duru za usalama nchini humo ni magaidi walioteka ndege kisha kuzigongesha katika jengo la Kituo cha Biashara cha Kilimwengu (World Trade Centre) na jengo lingine ambalo ndilo makao makuu ya ulinzi Marekani la pembe tano maarufu kama Pentagon.Tukio hilo liligharimu maisha ya watu wasio na hatia zaidi ya 2,996 huko Marekani.
Baada ya tukio hilo aliyekuwa rais wa Marekani wakati huo George W Bush alitangaza mwanzo wa vita alivyoviita kuwa ni Vita vya Msalaba (Crusade War)
Vita vilivyolengwa kupambana na mfumo (Ideology) ambavyo baadae vikaitwa vita vya kupambana na ugaidi huku Bush akilinyooshea kidole na kudai kundi la Al-Qaida lilihusika katika kupanga na kuratibu mashambulizi hayo na kuapa kuliangamiza kundi hilo popote lilipo.
Licha ya kundi la Al-Qaida kukanusha kuhusika kwake katika tukio Septemba 11, bado Marekani alitumia kura yake ya turufu (Veto power) kuivamia Afghanistan kwa madai ya kusaka magaidi ambao ilidai wameweka kambi nchini humo kwenye mji maarufu wa Kandahar. Aidha, Marekani chini ya Bush ilifanikiwa kuyashawishi mataifa mengine kuunga mkono vita kampeni yake hiyo ya vita dhidi ya ugaidi huko Afghanistan jambo lililopelekea Jumuiya ya Kujihami ya Nchi za Ulaya Magharibi (NATO) kuingia rasmi katika vita hivyo.
Katika hatua hiyo ya uvamizi nchini Afghanistan kulishuhudiwa uharibifu mkubwa wa uhai, mali na majereha pamoja na raia zaidi ya milioni moja wa Afghanistan kukimbia nchi yao, huku wazee watoto na wanawake wakitaabika.
Kuanzia kipindi hicho Vita vya kupambana na ugaidi vilipanua operesheni zake nyingi za kijeshi ikiwemo kuvamia Iraq, kwa kutumia vituo vyake vya kijeshi kutoka Qatar, Saudia nk. Bila ya kusahau kuwa jeshi la anga la Marekani kwa kutumia ndege zake maarufu zisizo na rubani aina ya drone zimekuwa zikipiga na kuuwa wasio na hatia na kujeruhi katika Pembe ya Afrika, nchi za Sahara, Mashariki ya Kati nk.
Kwa mujibu wa Shirika la Habari la Al-jazeera baada ya tukio la Septemba 11 lililopelekea uvamizi wa Afghanistan kisha Iraq kumepatikana zaidi ya vifo vya wahanga wasio na hatia zaidi ya1,690,903 nchini Iraq, wahanga 48,664 nchini Afghanistan na wahanga 35,000 ndani ya Pakistani
Aidha, Aljazeera imeongeza kuwa katika vita vya ugaidi Marekani na washirika wake wameweza kudondosha mabomu makubwa na makombora zaidi ya 326,000 katika maeneo ya Afrika ya Kaskazini na Mashariki ya Kati huku zikitumika fedha nyingi katika vita hivyo.
Katika miezi michache iliyopita wakati rais Biden akikhitimisha operesheni ya kijeshi Afghanistan iliyodumu kwa takriban miaka 20 alikiri kwa uchungu namna nchi yake ilivyogharamika zaidi ya kitita cha trioni 2.7 na kupoteza uhai wa askari wao kadhaa.
Tukio la Septemba 11 ni tukio tata lililojaa ulaghai, chuki na ambalo Marekani alilitumia kupata (legitimacy) uhalali wa kuua na kuupiga vita Uislamu na kutengeneza vikundi vya ugaidi feki ambavyo kazi yake ni kuupaka matope Uislamu. Kwakuwa tukio hili limejaa maswali tata ambayo mpaka leo yamekosa majibu hasa kwa wahanga waliopoteza ndugu zao katika tukio hilo ambao mwezi uliopita walimtaka rais Biden kuweka wazi nini hasa kilichotokea katika tukio hilo kutokana na taarifa za kutokea kwake kuwa na maswali mengi kama vile utekwaji wa ndege ulitokea vipi? Pia tangazo la rais Bush la Vita vya Msalaba kabla ya kupata ripoti rasmi na tukio kupotea kwa dola trion 3 katika makao ya ulinzi wa Pentagon punde tu baada ya kutokea kwa mashambulizi hayo. Zaidi aliyekuwa rais wa Marekani Donald Trump wakati wa kampeni zake za urais mwaka 2016 alimtuhumu Obama na Hilary Clinton kuhusika kutengeneza kikundi cha A-lQaida na ISIS, tuhuma ambazo idara za usalama nchini Marekani hazijawahi kuzikanusha.
Hiyo ndiyo Marekani, dola kubwa, kinara wa kuua na kupora rasilimali za nchi changa, kuleta machafuko, kuvuruga mshikamano katika jamii ili tu kufikia malengo yake ya kupata maslahi makuu.
وَإِذَا تَوَلَّى سَعَى فِي الأَرْضِ لِيُفْسِدَ فِيهَا وَيُهْلِكَ الْحَرْثَ وَالنَّسْلَ وَاللَّهُ لاَ يُحِبُّ الْفَسَادَ (البقرة: 205
“Na pindi wanapokwenda huku na kule huenda mbio kwenye ardhi kwa kufanya ufisadi ndani yake na kuangamiza mashamba na (kuteketeza) kizazi, na Allah hawapendi wenye kufanya ufisadi “
(Al-Baqara: 205)
Issa Nasibu.
Risala ya Wiki No. 112
11 Saffar 1443 Hijri / 18 Septemba 2021 Miladi

Maoni hayajaruhusiwa.