Maafa ya Maporomoko ya Ardhi kwenye Mlima Hanang: Somo Ambalo Halijazingatiwa

بسم الله الرحمن الرحيم

Habari:
Hadi kufikia tarehe 9 Desemba, 2023, idadi ya vifo kutokana na maporomoko ya ardhi hivi karibuni katika Mlima Hanang katika Mkoa wa Manyara, Tanzania viliongezeka hadi kufikia watu 85. Mbali na idadi kubwa ya vifo, maporomoko hayo yalisababisha nyumba nyingi kuharibika au kusombwa na maji, kuathirika miundombinu na watu wa eneo kuyahama makaazi yao.
Maoni:
Kufuatia maafa ya janga hili la kimaumbile asili lililotokea tarehe 2 Desemba, 2023 awali tunawapa pole familia zote za marehemu, na tunawafariji majeruhi wapone haraka ili hatimaye waendelee na maisha yao ya kawaida.
Majanga ya kimaumbile kama haya ni dhihirisho la wazi la udhaifu, utegemezi, kukosa udhibiti kwa wanadamu na vile vile kuwepo kwa Muumba ambaye anadhibiti kila nyanja ya maisha ya viumbe wake. Wanadamu walikuja katika maisha haya bila ya khiyari na wataondoka bila ya khiyari. Ni wajibu kwa kila mtu makini kutafakari kwa kina uhalisia huu na hivyo kupata majibu ya maswali nyeti zaidi ya maisha, kama vile: yeye nani, alikuwa wapi kabla ya kuja katika ulimwengu huu, nani aliyemuumba, nini kusudi la uumbwaji wake, atakuwa wapi baada ya kifo chake nk. Hapana shaka kwamba (anayejiuliza maswala hayo) atatambua kwamba kuna Muumba, Mmoja Pekee, Mwenye haki ya kuabudiwa.
Kwa upande mwingine, katika matukio kama haya yatokanayo na majanga ya kimaumbile kama maporomoko ya ardhi, licha ya kuwa ni miongoni mwa matendo ambayo ni matakwa ya Muumba (Al-Qadhaa) ambayo hatuna mamlaka ya kuyahoji, kwani kutokea kwake ni nje ya elimu, ujuzi na uwezo wa mwanadamu, lakini tunalazimika kuyawajibisha matendo yaliyo ndani ya mzunguuko/ uthibiti wa wanadamu, kama vile kudhibiti (madhara) na kuokoa mara tu janga linapotokea.
Tukitupia macho vitendo vilivyo ndani ya uwezo wa binadamu katika tukio hili kunaonekana wazi wazi kuwepo uzembe wa vyombo vya serikali na kutowajibika ipasavyo katika kushughulikia janga hili. Inasikitisha sana kwamba hakuna mipango madhubuti kabla ya kukabiliana na maafa, hakuna uwekezaji sahihi katika hatua za kujitayarisha na maafa, hakuna mifumo thabiti ya uokoaji, hakuna taasisi zenye uharaka kukabiliana na maafa na pia hakuna utaratibu thabiti wa kuelimisha Umma.
Ikumbukwe kuwa mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) ilitabiri mapema uwezekano wa hali ya mvua za msimu ambazo maeneo mengi ya nchi yanatarajiwa kupata mvua za juu ya wastani wa kawaida na za kawaida kuanzia mwezi wa Oktoba hadi Desemba 2023, ambazo zinatarajiwa kuathiriwa na hali ya El Niño. Ikiwa hali hizi zote na tahadhari zingezingatiwa, madhara hayangekuwa makubwa sana kama yalivyokuwa.
Zaidi ya hayo, hii si mara ya kwanza kwa mafuriko na maporomoko ya ardhi kusababisha vifo vya makumi ya watu nchini Tanzania. Tarehe 03 Disemba 2011, mvua kubwa iliyonyesha katika mikoa ya Kilimanjaro, Arusha na Mbeya ilisababisha maporomoko ya ardhi ambapo watu tisa walipoteza Maisha, na mamia kuachwa bila makaazi. Uwezekano huu wa maporomoko ya milima ulitosha kwa serikali kuchukua tathmini ya kina ya hatari na hatua madhubuti za kudhibiti maafa yajayo, lakini inaonekana dola haikujifunza kutokana na majanga yaliyopita.
Haya ndio maumbile ya nidhamu ya kidemokrasia katika mfumo wa kibepari ambao huwajali wanasiasa tu, wapambe wao na matajiri, huku wakipuuzilia mbali Umma. Tanzania kama sehemu yoyote duniani inahitaji Uislamu kama mfumo, kupitia dola yake ya Khilafah utaikomboa kutoka katika majanga na madhila, na kuweka mifumo yenye mikakati ya kukabiliana na maafa kwa haraka ili pia kujenga uwezo wa kukabiliana na majanga ya asili katika mustakbal.
Imeandikwa na Said Bitomwa
Mwanachama wa Afisi ya Habari ya Hizb ut Tahrir Tanzania
Kwa ajili ya Afisi Kuu ya Habari Hizb ut Tahrir

Maoni hayajaruhusiwa.