Ziara ya Blinken Nchini China

بسم الله الرحمن الرحيم

Swali:

CGTN (Chinese Global Television Network) ilichapishwa tarehe 30/6/2023: (Wizara ya Mambo ya Nje ya China iliikosoa Marekani kwa kutoa matamshi ya kutowajibika kuhusu uhusiano wa nchi hizo mbili. Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Anthony Blinken alisema katika mahojiano mapema kwamba Washington itaendelea kutetea maslahi yake binafsi, na itaendelea kuchukua hatua na kutoa matamshi ambayo China haiyapendi, bila kujali tofauti kati ya pande hizo mbili, na Wizara ya Mambo ya Nje ya China ilipinga taarifa hizi.) Kumbuka kwamba Al-Arabiya ilichapisha wiki moja kabla kwamba mnamo tarehe 23/6/2023: (Moja ya matarajio kutoka kwa ziara ya Blinken ni kwamba Waziri wa Hazina wa Marekani Janet Yellen atafanya ziara rasmi nchini China hivi karibuni, na Waziri wa Biashara Gina Raimondo na John Kerry, mjumbe wa tabianchi wa Biden, wanaweza pia kuzuru… Rais Xi pia ana uwezekano wa kuzuru San Francisco mnamo Novemba kuhudhuria mkutano wa Ushirikiano wa Kiuchumi wa Asia na Pasifiki, ambapo huenda akakutana na Biden). Ilitarajiwa kwamba uhusiano kati ya China na Marekani, baada ya ziara ya Blinken nchini China tarehe 18-19 ya mwezi wa Juni 2023, ungekuwa wa kutuliza uhusiano, na sio kwa hali kuregea tena katika mvutano! Je, ziara ya Blinken nchini China haikuwa na natija, au ilikuwa ni utaratibu wa kawaida tu? Samahani kwa urefu wa swali. Jazak Allah Khair.

Jibu:

Ili kupata jibu la wazi, hebu tuhakiki yafuatayo:

Kwanza: Mazingira yaliyo nyuma ya hali kuhusiana na ziara ya Blinken nchini China:

1- Hali ya mahusiano kati ya Marekani na China ni ya wasiwasi kwa kiasi fulani. Angalau tangu vita vya kibiashara vilivyoanzishwa na Rais wa zamani wa Marekani Donald Trump, serikali ya Marekani imeweka vikwazo mbalimbali kwa biashara na bidhaa za China, kuweka ushuru wa juu kwa baadhi ya bidhaa za China, na kuweka vikwazo kwa makampuni ya China kama vile Huawei na wakuu wake. Na sera hii haikubatilishwa na serikali ya Biden. Serikali ya China imejibu kwa sera sawa na hiyo. Hili pekee linatosha kuleta mvutano katika mahusiano kati ya nchi hizo mbili.

2- Wachina wamejitahidi kwa muda mrefu kujitegemea katika nyanja ya teknolojia chini ya mpango wa ‘Made in China 2025’, na zaidi ya hayo, jinsi Wamarekani walivyo amiliana na Huawei na makampuni mengine ya China ilileta mvutano ambao uliifanya China kupanga kuunda vipuri vyake yenyewe vya silicon. chips. Wachambuzi wa Marekani wanatarajia kwamba China itafikia, ndani ya miaka mitano hadi saba, uhuru katika sekta ya chip… Yote haya yanazalisha ushindani karibu na mgongano kati ya nchi hizo mbili.

3- Katika ngazi ya kijeshi na usalama, Februari iliyopita, puto la kijasusi la China lililoshukiwa kurushwa hadi anga ya Marekani, na ingawa China ilikanusha hili, jambo hili lilisababisha kubatilishwa kwa ziara ya Blinken jijini Beijing, ambayo ilipangwa kufanyika Februari iliyopita. Kisha, kukawa na mienendo ya meli za kivita za China katika Mlango wa Bahari wa Taiwan. Marekani ilijibu kwa kupeleka manuari kivita ya Marekani aina ya destroyer katika Mlango wa Bahari wa Taiwan mwezi uliopita, ikiizingatia Bahari ya China Kusini kama bahari huru ya kimataifa. Katika mwezi uliopita, ndege ya kivita ya China ilizikaribia ndege za Marekani, kisha anga kati ya nchi hizo mbili ikawa ya wasiwasi … Hivyo, ziara ya Blinken haikufanyika wakati huo.

4- Marekani imehitimisha mikataba mingi ya kijeshi na kiusalama ili kuihangaisha China, na utawala wa Biden umechukua msururu wa sera katika mwelekeo huu, ikiwa ni pamoja na mipango inayolenga kukabiliana na China kijeshi, hasa makubaliano ya AUKUS pamoja na Australia na Uingereza, na mazungumzo ya pande nne ya usalama pamoja na Australia, India na Japan. Pamoja na majaribio ya kupanua dori ya NATO barani Asia, Marekani ilihitimisha mkataba na Ufilipino wa kutumia kambi tano zaidi za kijeshi na kuwa kambi tisa nchini Ufilipino, na kwengineko.

Pili: Ama kuhusu ziara ya Blinken nchini China, haikuwa ni utaratibu wa kawaida, bali ilikuwa na malengo:

1- Jaribio la kupunguza mvutano unaotokana na mambo yaliyotangulia. Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani ilitoa taarifa na kusema kuwa lengo la ziara hii ni kufungua tena njia ya mawasiliano kati ya nchi hizo mbili ili kupata maelewano kati yao, na njia ya mawasiliano kati ya jeshi, na kufungua njia ya kuimarisha ushirikiano zaidi kati ya nchi hizo mbili… Pia ni wazi kutokana na taarifa hiyo, ziara ya Blinken ilifikia malengo, lakini haikufanikiwa kufikia mawasiliano baina ya wanajeshi.

2- Gazeti la Asharq Al-Awsat lililochapishwa mnamo Juni 19, 2023: (Licha ya lugha chanya iliyotumiwa na kiongozi wa China, akielezea kuridhika kwake baada ya mkutano wa dakika 35 na Blinken, wa pili aliweka wazi kuwa Beijing ilikataa kufungua tena njia za kijeshi na Washington, kwa kujua kwamba suala hili ni kipaumbele kwa utawala wa Rais Joe Biden, na ilikuwa moja ya malengo makuu ya ziara hii. Hata hivyo, mkutano huo uliofanyika katika Ukumbu wa Great wa Wananchi ulikuwa ni alama kwamba nchi hizo mbili hazitaki mahusiano yao kufikia uadui wa moja kwa moja, na kwamba wanatambua kwamba ushindani wao na jitihada zao za kidiplomasia zinabeba hatari kubwa).

3- Gazeti hilo liliongeza, [Baada ya siku mbili za mikutano na maafisa wakuu wa China, Blinken alisema kuwa Marekani iliweka malengo mahususi kwa ajili ya safari hiyo na kuyafanikisha, akionyesha kwamba aliibua suala la mawasiliano ya kijeshi “mara kwa mara.” Aliongeza, “Ni lazima kabisa tuwe na aina hizi za mawasiliano (…) Hili ni jambo ambalo tutaendelea kulifanyia kazi,” katika juhudi zilizoanza mnamo 2021 wakati China ilipokataa zaidi ya maombi mengi kutoka kwa Pentagon ya midahalo ya ngazi ya juu na upande wa China. Hata hivyo, Blinken alielezea majadiliano yake ya awali na maafisa wakuu wa China kuwa “ya wazi na yenye kujenga” (Gazeti la Al-Sharq Al-Awsat, 19/6/2023)].

4- Kwa hivyo, moja ya maswala makuu ambayo hayajatatuliwa ni kuregeshwa kwa mawasiliano ya kijeshi kati ya Marekani na China. Mawasiliano kati ya maafisa wakuu wa kijeshi kati ya nchi hizo mbili bado yamekwama, na matukio mawili ya hivi majuzi yameibua hofu kwamba uhusiano huo uliodorora unaweza kuzua mzozo. Hivi karibuni China ilikataa mkutano kati ya Waziri wa Ulinzi wa Marekani Lloyd Austin na Waziri wa Ulinzi wa China Li Shangfu nchini Singapore… Blinken alisema kuwa ingawa aliibua haja ya njia hizo “mara kwa mara” katika mikutano yake, “hakuna maendeleo ya haraka”. Kwa sasa, China haijakubali kuendelea mbele nayo. Nadhani hilo ni suala ambalo tunapaswa kuendelea kulifanyia kazi,” aliongeza. Alisema, “Ni muhimu sana turegeshe chaneli hizo” (CNN, 19/6/2023)

5- Hakuna shaka kwamba ziara ya Blinken ilifanya maendeleo fulani. Lakini kama Blinken alivyosema, maendeleo hayajawa rahisi. [“Uhusiano ulikuwa katika kipindi cha kukosekana kwa utulivu, na pande zote mbili zilitambua haja ya kufanya kazi katika kuleta utulivu,” Blinken alisema kabla ya kuondoka China. Aliongeza: “Lakini maendeleo ni magumu. Inachukua muda. Si zao la ziara moja, au safari moja, au mazungumzo mamoja. Matumaini yangu na matarajio yangu ni: Tutakuwa na mawasiliano bora, ushirikiano bora zaidi katika siku zijazo.” Aliongeza, “Maafisa wa Marekani wamekuwa wakipuuza uwezekano wa mafanikio makubwa, lakini wanatumai ziara ya Blinken itafungua njia kwa mikutano zaidi ya nchi hizo mbili, ikiwa ni pamoja na safari zinazowezekana za Waziri wa Hazina Janet Yellen na Waziri wa Biashara Gina Raimondo. “Ilitarajiwa kwamba hii ingefungua njia kwa mkutano wa kilele kati ya Xi Jinping na Biden baadaye mwaka huu.” (Reuters, 20/6/2023)].

6- Kuhusu suala la vita vya Ukraine, Al-Jazeera Net ilichapisha: [Blinken alikaribisha mapendekezo ya China ya amani ya kudumu nchini Ukraine, na kusema kuwa China ilithibitisha kwamba haikutoa msaada wowote kwa Urusi katika vita vyake dhidi ya Ukraine, akibainisha, hata hivyo, hofu yake “kuhusu ushiriki wa makampuni ya Kichina katika hilo.” (Al-Jazeera Net, 19/6/2023)]. Blinken alisema: [China imeihakikishia Marekani na nchi nyingine kwamba haitatoa msaada wa mauaji kwa Urusi na “hatujaona ushahidi wowote wa kinyume chake,” ingawa alibainisha kuwa uhakikisho wa China unaambatana na taarifa za mara kwa mara zinazotolewa katika wiki za hivi karibuni. (CNN IN, 19/6/2023)].

7- Kuhusu suala la Taiwan, Gazeti la Al-Sharq Al-Awsat lilichapisha kwamba waziri wa China [“alisisitiza kwa mara nyingine msimamo wa nchi yake kwenye faili ya Taiwan, na kuhusu kile ambacho Beijing inakiona kuwa ni maelewano ya kuendelea katika miaka ya hivi karibuni kati ya Washington na mamlaka za Taiwan yanayotokana na upande unaounga mkono uhuru wa kisiwa hiki.” Chen Gang alisema, kwa mujibu wa taarifa iliyoripotiwa na wizara yake: “Suala la Taiwan ni kiini cha maslahi msingi ya China, suala muhimu zaidi katika uhusiano wa China na Marekani na hatari kubwa zaidi.” Alisisitiza kwamba “China inaitaka Marekani kuheshimu kanuni ya China-Moja”; yaani, kutoanzisha uhusiano rasmi na Taiwan, “na kuheshimu ahadi yake ya kutowaunga mkono watenganishaji wa Taiwan”. Kwa upande wake, afisa mkuu wa mambo ya nje wa China, Wang Yi, alimhakikishia Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani kwamba nchi yake haitafanya “makubaliano yoyote” juu ya Taiwan.” (Middle East, 19/6/2023)].

Kwa upande wake, Blinken alisema [Nchi yake haiungi mkono uhuru wa Taiwan, na inatarajia suluhisho la amani kwa suala hilo, akiashiria kwamba makubaliano yao na China “yamejikita katika kutafuta suluhisho la amani kuhusiana na mizozo yoyote inayohusiana na Taiwan, na tunaunga mkono China moja.” (Al-Jazeera Net, 19/6/2023)]. Tovuti ya BBC iliripoti taarifa ya Blinken kwamba [“kuna wasiwasi unaoongezeka kuhusu “vitendo vya uchochezi” vya China katika Mlango-Bahari wa Taiwan, lakini anasisitiza kwamba Marekani haiungi mkono uhuru wa Taiwan. Anasema kwamba ikiwa kutakuwa na mgogoro juu ya Taiwan, pengine “itasababisha mgogoro wa kiuchumi ambao unaweza kuathiri dunia nzima”. Alifafanua kuwa 50% ya trafiki ya makontena ya kibiashara hupitia Mlango-Bahari wa Taiwan kila siku. Na 70% ya mauzo ya semiconductor hufanywa nchini Taiwan. (BBC, 19/6/2023)].

Tatu: Kutokana na haya yote, yafuatayo yanadhihirika:

1-Hakuna mabadiliko katika msimamo wa Marekani kuelekea Taiwan… Marekani haijatambua uhuru wa Taiwan (ikibainisha kuwa kuna takriban nchi 15 zinazotambua rasmi uhuru wa Taiwan, ikiwemo Vatican). Ingawa Marekani haikuamua kutambua rasmi uhuru wa Taiwan, inaichukulia Taiwan kama nchi huru, kama inavyothibitishwa na ukweli kwamba kuna afisi ya Marekani huko Taipei ambayo inafanya kazi kama ubalozi wa Marekani, na Marekani imehitimisha makubaliano ya ulinzi na Taiwan na kuipatia aina ya silaha za hali ya juu, na usaidizi mwingine. Marekani inatangaza kuilinda Taiwan katika tukio la shambulizi la kijeshi kutoka China, na Biden alithibitisha hili Mei mwaka jana. Rais wa Marekani Joe Biden alionya kwamba “China inacheza na moto katika suala la Taiwan” na kuahidi kuingilia kijeshi ili kulinda kisiwa hicho ikiwa kitashambuliwa. (BBC, 23/5/2022).

2- Ziara hii na “matokeo” yake hayatoshi kutuliza hali ya anga baina ya nchi hizi mbili, bali inaweza kuwa ni upenyo wa muda wa mlango wa utulivu baina yao na utangulizi wa ziara nyingine… Kama ilivyoelezwa katika swali moja ya matarajio kutoka kwa ziara ya Blinken (kwamba Waziri wa Hazina wa Marekani Janet Yellen atafanya ziara rasmi nchini China hivi karibuni. Waziri wa Biashara Gina Raimondo, pamoja na John Kerry (mjumbe wa hali ya hewa wa Biden), wanaweza pia kutembelea, ikizingatiwa kwamba wote wawili wanawajibika kwa masuala ambayo yanazifunga China na Marekani katika maslahi ya pamoja ili kushirikiana. Inawezekana pia kwamba Rais Xi atazuru San Francisco mwezi Novemba kuhudhuria mkutano wa Ushirikiano wa Kiuchumi wa Asia na Pasifiki, ambapo anaweza kukutana na Biden.) Lakini hilo halimaanishi kwamba mlango wa mvutano kati ya nchi hizo mbili umefungwa na mlango mpya wa mapatano ya kudumu umefunguliwa kati ya nchi hizo mbili. Hii haiwezekani kwa sababu maslahi yao ni tofauti … washirika wa Marekani pambizoni mwa China kama vile Japan, Korea Kusini, Ufilipino, na kisha suala la Taiwan … Wote hawa watazuia mlango wa mvutano kufungwa, bali utabaki wazi kufunguliwa tena kwa mujibu wa maslahi ya nchi hizo mbili.

3- Lakini moja ya malengo muhimu ya ziara hii ambayo halikufikiwa ni kwamba Marekani ilitaka kufungua njia ya mawasiliano kati ya jeshi la China na Marekani, kwa malengo sawa na ujasusi! Kana kwamba China iligundua hilo, ilikataa njia hizi kimsingi, na hii ndio iliyomkasirisha Blinken, hata ikiwa hakuonyesha wazi, lakini alikuwa wazi katika maneno na taarifa zake, kama tulivyoelezea hapo juu, na nitazikumbusha tena:

* (Licha ya lugha chanya iliyotumiwa na kiongozi wa China, akielezea kuridhika kwake baada ya mkutano wa dakika 35 na Blinken, wa pili aliweka wazi kwamba Beijing ilikataa kufungua tena njia za kijeshi na Washington, akibainisha kuwa suala hili ni kipaumbele kwa utawala wa Rais Joe Biden, na ilikuwa moja ya malengo makuu ya ziara hiyo).

* (Baada ya siku mbili za mikutano na maafisa wakuu wa China, Blinken alisema kwamba Marekani ilikuwa imejiwekea na kufikia malengo mahususi kwa ajili ya safari hiyo, akibainisha kwamba alikuwa amezungumzia suala la mawasiliano ya kijeshi “mara kwa mara.” Aliongeza, “Ni muhimu mno kwamba tuwe na aina hizi za mawasiliano (…) Hili ni jambo ambalo tutaendelea kulifanyia kazi”).

* (Matukio mawili ya hivi majuzi yameibua wasiwasi kwamba uhusiano huo uliodorora unaweza kuingia kwenye mzozo. Hivi majuzi China ilikataa mkutano kati ya Waziri wa Ulinzi wa Marekani Lloyd Austin na Waziri wa Ulinzi wa China Li Shangfu nchini Singapore… Blinken alisema kuwa ingawa aliibua haja ya njia kama hizo “kwa njia ya maana tena na tena” katika mikutano yake, lakini “hakukuwa na maendeleo ya haraka.”

“Kwa sasa, China haijakubali kuendelea mbele nayo. Nadhani hilo ni suala ambalo inabidi tuendelee kulifanyia kazi,” aliongeza. “Ni muhimu sana turegeshe chaneli hizo,” alisema.

4- Pengine misimamo hii kutoka China ilibaki imekwama akilini mwa Blinken kwa sababu hakuweza kukamilisha mawasiliano ya kijeshi, hivyo taarifa zake za mwisho zilitajwa kwenye swali… pamoja na zile zilizoripotiwa na tovuti ya Saba mnamo tarehe 29/6/2023: (Shirika jipya la habari la China Xinhua limemnukuu msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya China, Mao Ning, akijibu taarifa za Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Anthony Blinken akisema: “Siyo siri kwamba kuna tofauti kati ya Marekani na China.” Aliongeza: “Kile Marekani ilichokisema na kukifanya kinakiuka sheria msingi zinazosimamia mahusiano ya kimataifa” … akisisitiza upinzani wa nchi yake kwa suala hili …). Mwenyezi Mungu Al-Qawwi Al-Aziz ndiye Mkweli:

[وَكَذَلِكَ نُوَلِّي بَعْضَ الظَّالِمِينَ بَعْضاً بِمَا كَانُوا يَكْسِبُونَ]

“Ndio kama hivi tunawaelekeza madhaalimu wapendane wao kwa wao kwa sababu ya waliyo kuwa wakiyachuma.” [Al-An’am: 129].

[وَالْكَافِرُونَ هُمُ الظَّالِمُون]

“Na makafiri ndio madhaalimu.” [Al-Baqarah: 254].

15 Dhul Hijjah 1444 H

3/7/2023 M

Maoni hayajaruhusiwa.