‘Wendawazimu’ Katika Sherehe za Mwaka Mpya

بسم الله الرحمن الرحيم

وَمَا كَانَ صَلاَتُهُمْ عِنْدَ الْبَيْتِ إِلاَّ مُكَاءً وَتَصْدِيَةً فَذُوقُوا الْعَذَابَ بِمَا كُنتُمْ تَكْفُرُونَ
‘Na haikuwa ibada yao kwenye hiyo nyumba (kaaba) ila ni kupiga miunzi na makofi(kelele). Basi onjeni adhabu kwa vile mlivyokuwa mkikufuru’ (TMQ 8:35)

Miongoni mwa ibada za Maqureishi katika zama za jahilliya ilikuwa ni kupiga makelele, makofi, kutufu uchi, na kila aina ya uovu katika masiku ya Hijja. Na shetani aliwapambia uovu wao huo kwa kujiona wanatenda wema. Uislamu ukaja ukawakomboa na matendo hayo ya ‘ujendawazimu’ na ukawapangia ibada inayowafikiana na maumbile yao kukidhi ghariza/hisia ya kuabudu. Aidha, Uislamu uliwakuta na sikukuu na sherehe mbali mbali walizojiwekea, ukaziondoa na kuwawekea sikukuu maalum na namna maalum ya kusherehekea, kwa vipimo vya ‘halali’ na ‘haramu’ na kwa namna ya kuzishukuru neema za Allah Ta’ala mara baada ya kumalizika ibada tukufu ya Hijja na kumalizika saumu ya mwezi mtukufu wa Ramadhani.

Leo chini ya mfumo wa kidemokrasia ‘uwendawazimu’ wa kupiga makelele na kufanya vitendo vya fujo na ufuska katika ‘ibada ya sherehe za mwaka mpya’ unaendelea kupamba moto kila mahali hususan katika nchi za Magharibi zinazoitwa zimeendelea na kustaarabika, na pia katika nchi zetu changa zinazoburuzwa na thaqafa/mila chafu na potofu za za kimagharibi. Na kwa hakika uovu wa leo ni mkubwa na hatari zaidi kwa ustawi wa wanaadamu hata kuliko ule wa waarabu katika zama za kiza na ujahillia. Uovu huu wa kufanya vitendo vya uwendawazimu ati kwa kusherehekea kuingia mwaka mpya ulioshitadi zaidi katika mataifa ya Magharibi unatokana na mambo mawili makubwa:

Kwanza, hii ni katika athari ya kuziba uwazi mkubwa (vacuum) uliopo wa hitajio la kiibada ndani ya nafsi za raia wa nchi hizo, ambao wengi wao kama si wote hawana namna ya kuliziba pengo hilo kutokana na mfumo wao wa kidemokrasia kuwaonesha dini ni kitu duni. Kwa sababu mwanaadamu ana hisia ya ndani ya kimaumbile inayomsukuma kuhitajia ibada fulani kwa ajili ya kumtukuza Muumba wake (ghariza ya kuabudu). Kwa hivyo, anapokosa mwanaadamu ibada sahihi kukidhi kiu yake hiyo ya kimaumbile, hujibunia ibada yake mwenyewe au hubuniwa na wengine ili kukidhi kiu yake hiyo ya kimaumbile. Ukiangalia kwa makini, namna ya sherehe hizi zinavyofanywa katika nchi za Magharibi, kimsingi japo kwamba kidhahiri utaona ni sherehe lakini kwa umbali wake zimefanywa kuwa ‘ibada ya kuingia mwaka mpya’. Aidha, ukiangalia namna watu wa magharibi wanavyowatukuza, kuwaenzi na kuwanyenyekea watu wao maarufu (celebrities) kama wanamuziki, wacheza filamu, wacheza mpira nk. Unyenyekevu ambao huwezi kuamini kwa mwanaadamu kudiriki kumfanyia mwanaadamu mwenzake anaekula, kwenda haja, kuumwa na hatimae kufariki. Lakini kwa umbali, jambo hili huwa ni kutokana na msukumo wa ghariza hii ya ibada. Kwa kuwa asili Mwenye haki ya kutukuzwa, kunyenyekewa na kuenziwa katika kiwango hicho ni Muumba pekee. Na kwa kuwa watu hawa wamekwenda kombo na njia ya haki, na kuikosa ibada sahihi, ilhali ghariza ya ibada kimaumbile inatokota nafsini mwao, hapana shaka ghariza hiyo hutafuta njia ya kutokea. Na badala yake watu hawa badala ya kumnyenyekea Muumba wa haki, humalizikia kunyenyekea, kutukuza, kuwaenzi watu maarufu (celebrities). Kiasi cha kutokea matukio ya ajabu! kama vile mashabiki (wafanya ibada) kuwahi kukesha nje ya vipenu vya hoteli aliyofikia Michel Jackson alipofanya ziara ndani ya jiji la London, huku maskini! mashabiki (wafanya ibada)wakiandamwa na baridi kali isiyomithilika.

Jambo la pili ni msukumo wa fikra zao potofu za kikafiri za ‘uhuru binafsi’ (personal freedom) zinazotokamana na nidhamu yao ya kikafiri ya kidemokrasia. Kwa kuingia mwaka mpya wao huona ni muda muwafaka wa kufanya kila aina ya uchafu kama kulewa, kuzini, kufanya liwati, kufanya vitendo vya usagaji, kupiga makelele kwa honi za magari inapoingia saa sita na dakika moja usiku, makelele ya magoma, mikusanyiko ya mchanganyiko ya wanawake na wanaume, kwenda utupu wa mnyama nk. Yote hayo kwa kisingizio cha kuutumia ‘uhuru wao’ wa kibinafsi kwa kusherehekea usiku wa kuingia mwaka mpya. Kwa bahati mbaya na hata baadhi ya Waislamu kimakosa hujiingiza katika aina hii ya ujahilia katika kusherehekea kuingia mwaka mpya wa kalenda ya miladia na kujiingiza katika vitendo vichafu vya haramu. Tunawanasihi kwa ikhlasi waache mara moja.

Kalenda ya miladia iliasisiwa tangu zama za utawala wa Himaya ya waroma chini ya mtawala Julius Caesar miaka ya 150 BC. Na katika mwaka 1582, Pope Gregory xiii aliimakinisha zaidi kalenda hiyo na kuitia sura rasmi, na ndio maana baadhi wameipa jina kalenda hii kwamba ni ‘kalenda ya Gregory’ (Gregorian calendar) Zama zote hizo sherehe mbalimbali zilikuwa zikifanywa kuukaribisha mwaka mpya, zilizoambatana na vionjo vya kidini na mila za kipagani. Na ubepari/uarasilmali ulipopata nguvu ndani ya Ulaya na Marekani waliendelea kuitumia kalenda hiyo na pia kuendelea kufanya sherehe maalum za kuingia mwaka mpya. Hata hivyo, sherehe hizi za mwaka mpya zilianza kupata nguvu zaidi katika karne ya 19 wakati raia wa Marekani walipokuwa wakikusanyika kusherehekea katika viwanja vya miji mikuu kama New York, Philadelphia, Baltimore nk. Na mtindo huo kuanza kuenea katika miji mikuu mbali mbali ndani ya Ulaya na nje ya Ulaya.

Kwa hivyo, imekuwa ni ada ya wanademokrasia kutokana na fikra zao chafu kufanya kila aina ya ufuska katika kusherehekea kuingia mwaka mpya. Na uchafu huo hutendwa mbele ya macho ya serikali zao, na raia wao kukusanyika katika viwanja vikubwa kwa ajili ya sherehe hizo. Serikali zao huwaachia huru, kwa kuwa kwanza hunufaika kiuchumi, kwa kuwa siku hii imekuzwa sana kama ni siku tukufu kiasi cha kufanywa ni siku ya mapumziko (public holiday) katika nchi nyingi. Na raia wao hujiingiza gharama zisizokuwa za lazima kwa ajili ya kusherehekea mwaka mpya. Lakini pia serikali zao zinaifanya sherehe hii miongoni mwa mbinu ya kuwapumbaza raia wao ili wapunguze joto la kubanwa na mfumo wao muovu wa kibepari. Na kubwa zaidi, wanademokrasia hudai kwamba kazi ya serikali za kidemokrasia ni kulinda na kudhamini uhuru wa mtu binafsi.

Uislamu umekuja kumuwekea mwanaadamu ibada maalum ili kukidhi na kukinaisha hisia zake za kimaumbile. Aidha, umeweka sherehe maalum zinazoambatana na vipimo vya ‘halali’ na ‘haramu’ katika kusherehekea sherehe hizo. Kamwe Uislamu hauwaachii wanaadamu kuwa kama wanyama mbugani kufanya wanayotaka kwa kisingizio cha ‘uhuru’. Fikra chafu zinazomuangamiza binaadamu leo. Kadhalika Uislamu ukaichukulia neema ya umri/wakati miongoni mwa neema kubwa ambayo kamwe si ya kubezwa wala kutumiwa kwa vitendo vya fujo na ufuska. Bali unamtaka mwanaadamu kujifunga katika umri wake wote kumcha Allah Ta’ala. Mtume SAAW alimuusia sahaba Abudhar al- Ghifari na umma mzima kwa kusema:

“Ewe Abu dhar ,faidika na vinne kabla ya vinne: ujana wako kabla ya uzee wako, na siha yako kabla ya maradhi yako, na wasaa wako kabla ya ufukara wako, na uhai wako kabla ya mauti yako.”

Masoud Msellem
31 Disemba 2021

 

Maoni hayajaruhusiwa.