Mazazi ya Mtume (Saw) Yatuunganishe na Sio Kutufarakanisha

بسم الله الرحمن الرحيم

Amesema Allah (Swt):
(كُنتُمْ خَيْرَ أُمَّةٍ أُخْرِجَتْ لِلنَّاسِ تَأْمُرُونَ بِالْمَعْرُوفِ وَتَنْهَوْنَ عَنِ الْمُنكَرِ وَتُؤْمِنُونَ بِاللّهِ)
“Nyinyi mmekuwa bora ya Ummah waliotolewa watu. (Kwa kuwa) mnaamrisha mema na mnakataza maovu, na mnamuamini Mwenyezi Mungu.” [Aal-Imran: 110]
Kwa kipindi cha zaidi ya karne 13 ulimwengu wa Kiislamu ukiwa chini ya dola ya Khilafah uliishi ukiwa na hadhi ya juu mbele ya jamii nyengine duniani.
Katika kipindi hicho dola ya Kiislamu iliweza kuunganisha jamii za watu wa mataifa mbalimbali, wenye lugha, tamaduni, mila na desturi tafauti na kuwafanya kitu kimoja, wakiwa na udugu na upendo chini ya bendera ya Laa ilaaha illa llaah Muhammada-Rrasulullah.
Iliweza dola kusimamia na kuboresha ustawi wa hali za kimaisha kwa raia wake na kusimamia haki na sheria kwa usawa na uadilifu baina ya watu wote bila kutofautisha baina ya watawala na watawaliwa, matajiri na masikini au wenye hadhi na wasio na hadhi katika jamii.
Aidha, dola ililinda heshima na utu kwa wote, wakiwa wanawake, wanaume, watoto, Waislamu na wasiokuwa Waislamu.
Hii ndio risala na ujumbe wa Mtume wetu Muhammad (saw) aliotuletea na kuanza yeye Mtume SAAW kutuonyesha kivitendo namna Ummah wetu unavyotakiwa kuishi. Pia Saaw aliweza kuwaunganisha wanadamu (Waislamu na wasioukuwa Waislamu) wakiwa ni Ummah mmoja ulio na kiongozi mmoja, utawala mmoja na chini ya bendera moja.
Hali hiyo ni kinyume na iliyopo sasa katika miji yetu chini ya mfumo dhalimu wa kibepari. Leo kunashuhudiwa ubaguzi, chuki, uhasama, baina ya wanajamii, uporaji wa rasilmali unaofanywa na mabepari wachache, wakoloni na vibaraka wao. Wakichochea chuki na uhasama baina ya Waislamu na jamii zetu huku wao wakiendelea kunufaika kutokana na kukosa kwetu umoja na mshikamano.
Katika mwezi huu wa Rabi ul Awwal aliozaliwa kiongozi wetu Mtume (saw) ni jukumu letu kuhakikisha tunajifunga na ufaradhi wa kuirejesha tena jamii ya Kiislamu kwa kusimamisha tena dola ya Kiislamu ya Khilafah kwa kuanzia katika nchi kubwa za Kiislamu. Dola hiyo pekee ndio yenye uwezo kuirejesha tena hadhi yetu tukiwa Ummah ulioungana na sio kufarakana.

Maoni hayajaruhusiwa.