Zanzibar Inahitaji Mabadiliko Ya Kimsingi Kukabiliana Na Mporomoko Wa Maadili

بسم الله الرحمن الرحيم

 

Taarifa kwa Vyombo Vya Habari

Kutokana hatua ya Baraza la Sanaa, Sensa ya Filamu na Utamaduni la Zanzibar kumzuiya kwa miezi sita Zuchu, mwimbaji mziki wa Bongo fleva asifanye maonesho yake Zanzibar kuanzia tarehe 5 Machi 2024 kufuatia uimbaji wake usio na maadili katika onesho la Full Moon Kendwa Night Show lililofanyika kaskazini mwa Zanzibar mnamo tarehe 24 Februari 2024, sisi Hizb ut Tahrir /Tanzania tungepependa kusema yafuatayo:
Wakati adhabu ya Baraza kwa Zuchu ni kitu cha kuthaminiwa, bado ni hatua nyepesi na ya kijanjajanja kwa kutilia maanani mambo mawili:
Awali, zuiyo la miezi sita kwa Zuchu likiambatana na faini ya TSh milioni moja ($375) na kutakiwa kuwasilisha ombi la msamaha kwa maandishi ni adhabu hafifu kufidia makosa makubwa ya kimaadili aliyoyatenda katika onesho lake.
Pili, maonesho ya mziki unaoitwa ‘bongo fleva’ kimaumbile hayana maadili kwa sura yoyote iwayo, yawe maonesho hayo ya Zuchu au mwengine yoyote, na kwa hakika maonesho hayo yanagongana moja kwa moja na silka, desturi na utamaduni wa Zanzibar ambapo takribani wakaazi wake wote ni Waislamu. Hivyo, qadhia hapa (kwa baraza) sio kuzuiya jambo hilo kwa muda, bali ni kulikataza moja kwa moja.
Aidha, tunapenda kulikumbusha na kulionya baraza ambalo linadai kujitwisha dhamana ya kulinda na kuhifadhi mila, desturi na utamaduni wa Zanzibar ambazo bila ya shaka ni Uislamu, pia tunazikumbusha na kuzionya taasisi nyengine zenye majukumu kama hayo (kama baraza) kwamba Zanzibar ambayo huko nyuma ilikuwa taa iliyoangazia nuru kwa ustaarabu na maadili, leo imegeuka kuwa ngome ya aina zote za uovu usio na maadili ukihamasishwa na serikali na taasisi zake kwa kisingizo cha ‘uhuru binafsi’, ‘uwekezaji’ na kuimarisha sekta ya utalii.
Matokeo yake Zanzibar imedidimia katika shimo la ina kirefu lenye kila aina ya uovu, mporomoko wa maadili na uchafu, kama ushoga, zinaa, usagaji, ukatili wa kijinsia, ulevi, madawa ya kulevya nk. Yanatendeka hayo ilhali taasisi za serikali zikichangia au zikikodolea macho bila ya kuchukua hatua zozote stahiki, wakisubiria maangamizi zaidi kwa vizazi vyetu katika mustakbal.
Kwa ukweli, Zanzibar chini ya mfumo wa kibepari haiwezi na haitoweza kwa udhati kukabiliana na mporomoko wa maadili, kwa kuwa msingi wa roho ya ubepari ni kukosekana maadili.
Jambo hilo la (kukabiliana na mporomoko wa maadili) linaweza kufanikiwa tu kwa mabadiliko ya kimsingi ya Uislamu chini ya usimamizi wa dola yake ya Khilafah inayostahiki kuasisiwa kwa kuanzia katika ulimwengu wa Kiislamu. Kwa dola hiyo (Khilafah) maovu yote na mporomoko wa maadili yatakomeshwa kimsingi kwa ustawi wa Waislamu na wanadamu kwa jumla.
Masoud Msellem
Mwakilishi kwa Vyombo vya Habari Hizb ut Tahrir Tanzania
KUMB: 1445/04
Ijumaa, 27 Shaaban 1445 Hijria
08 Machi 2024 Miladi

Maoni hayajaruhusiwa.