Ongezeko la Kodi katika Nishati ya Mafuta Kutaathiri Zaidi Maskini

بسم الله الرحمن الرحيم

Habari:

Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji nchini Tanzania (EWURA) imetoa kikomo cha bei mpya za jumla na reja reja za bidhaa za mafuta ya petroli ambazo zitaanza kutumia kuanzia Alkhamisi tarehe 01/07/2021, kufuatia marekebisho ya Sheria ya Fedha ya mwaka 2021 ambayo imetoa ruhusa ya kuongezwa kodi kiasi cha Tsh 100 kwa kila lita ya mafuta ya petroli, dizeli na mafuta ya taa.

Maoni:

Bei hizi mpya zimekuja kama chanzo kipya cha mapato ya serikali kufuatia ombi la serikali wakati ilipowasilisha bajeti ya taifa kwa mwaka wa fedha 2021/2022. Kwahiyo, Sheria ya Fedha ya mwaka 2021 ikarekebishwa na bunge ili kutoa ruhusa ya kuwekwa kwa bei mpya.

Chini ya bei hizi mpya, jumla ya kodi za serikali zinapaa mpaka Tsh 892.00 katika kila lita moja ya petroli. Hii inajumuisha Tsh 413.00 (Fuel levy), Tsh 379.00 (Excise Duty), na Tsh 100 (Petroleum fee) na bado kuna makato mengine, kama vile kodi za mamlaka za usimamizi (executive agencies), kodi zinazolipwa kwenye serikali za mitaa nk. Hii inamaanisha kuwa mfanyabiashara wa rejareja wa mafuta atapata faida ya Tsh 129.10 kwa kila lita, ilhali serikali itakomba hadi Tsh 892.00.

Kwa mujibu wa EWURA, kufuatia kuongezeka kwa kodi mpya za nishati, bei mpya za jumla itakuwa ni Tsh 2275.90 kwa petroli, Tsh 2086.00 kwa dizeli na Tsh 1992.51 kwa mafuta ya taa, wakati bei za rejareja itakuwa ni Tsh 2405 kwa petroli, Tsh 2215 kwa dizeli na Tsh 2121 kwa mafuta ya taa katika jiji na mikoa ya karibu. Kwa baadhi ya mikoa ya mbali kama vile Kigoma, bei ya rejareja itapanda mpaka kufikia Tsh 2649 kwa petroli, Tsh 2459 kwa dizeli na Tsh 2365 kwa mafuta ya taa kwa kila lita moja.

Hali hii inafedhehi zaidi uwepo wa sera za kiuchumi mbovu na za katili, kwani baadhi ya nchi za jirani zisizo na bandari kama Zambia na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) ambazo hupitishia mafuta yao Tanzania kupitia bandari ya Dar es Salaam wana bei nafuu kuliko bei ya mafuta ya Tanzania, ambapo nchini Zambia bei ya lita moja ya mafuta ya petroli ni Kwacha 17.60 (Tsh 1900) na nchini Congo DRC ni Franc 1800 (Tsh 2087).

Kuongezeka kwa bei ya mafuta kutaongeza maumivu zaidi na kusababisha mfumuko wa bei katika bidhaa na huduma zinazogusa maisha ya watu wengi masikini na madhaifu. Hivyo, bidhaa za viwandani, vyakula, mazao ya kilimo na huduma za usafirishaji zote zitaongezeka bei.

Zaidi ya hayo, hatua hii pia itawaathiri wafanyabiashara wa mafuta na kusababisha uhaba usio wa lazima wa nishati hiyo kutokana na ukweli kuwa wafanyabiashara wanaweza kujihusisha na njia za panya ili kulinda biashara zao.

Hivi ndivyo ulivyo uovu na ukatili wa wanasiasa wa kidemokrasia, wakiwemo wabunge ambao wanapata mishahara minono kutokana na pesa za walipa kodi, lakini hawawajali hao wanaodai kuwawakilisha, kiasi cha kufanya marekebisho ya Sheria ya Fedha ya mwaka 2021 wakati wanajua fika itaongeza mateso na ugumu kwa masikini walio wengi.

Hili ni kofi la fedheha usoni kwa watu masikini ambao (wabunge) hudai wanawawakilisha, na pia ni ushahidi tosha kuwa wanasiasa wa kidemokrasia hawapo kuwatumikia watu, bali kutumikia maslahi yao binafsi.

Inashangaza kuwa ongezeko la kodi katika bidhaa za mafuta ya petroli imebuniwa kama njia ya kuongezea mapato ya serikali kufuatia madhara ya kiuchumi yaliyosababishwa na Covid 19. Hata hivyo, miezi michache nyuma katika kipindi cha utawala wa Raisi (aliyefariki) John Magufuli tuliambiwa kuwa Tanzania hakuna Covid 19, na uchumi haujaathiriwa na janga hilo.

Ni zaidi ya majonzi kwa nchi zinazoendelea kama Tanzania, kuwa pamoja na kumiliki utajiri mwingi kama vile maliasili na madini lakini bado kwa kukosekana mfumo wenye nuru (Uislamu) na kutokana na uwepo wa unyonyaji wa kibepari wa mataifa ya Magharibi, zimeshindwa nchi (zinazoendelea) kufaidika na utajiri wake, kiasi kwamba huona suluhisho pekee la kuongeza mapato ya serikali ni kubuni aina mpya za kodi ambazo zinazidisha ugumu wa maisha kwa walio wengi.

Nchi zinazoendelea na ulimwengu kiujumla zinahitaji mfumo wenye uadilifu ambao ni Uislamu, kupitia serikali yake ya Khilafah itawakomboa wanadamu kutokana na mfumo muovu, wa kikatili na wa kinyonyaji wa kibepari, na kuwapeleka katika ustawi wa kweli wa maisha ya duniani na akhera.

Imeandikwa na Said Bitomwa

Mwanachama wa Afisi ya Habari ya Hizb ut Tahrir Tanzania

Kwa ajili ya Afisi Kuu ya Habari ya Hizb ut Tahrir

Maoni hayajaruhusiwa.