Wachache Wameachiwa Huru, Lakini Mahabusu Wengi Bado Wanateseka Vizuizini

بسم الله الرحمن الرحيم

Habari:

Mnamo tarehe 04/03/2022, kiongozi wa chama kikuu cha upinzani nchini Tanzania, Freeman Mbowe na watuhumiwa wenzake watatu waliachiliwa huru baada ya Mkurugenzi wa Mashtaka kufuta mashtaka ya ugaidi dhidi yao. Muda mfupi kabla ya kuachiliwa akina Mbowe, tarehe 23/02/2022, wanachama watatu wa Hizb ut Tahrir Tanzania Ust Ramadhan Moshi Kakoso (45) Waziri Mkaliaganda (37) na Omar Salum Bumbo (55) pamoja na baadhi ya watuhumiwa wengine Waislamu waliokuwa wamebambikiwa kesi za ugaidi na kuwekwa kizuizini kwa miaka mingi nao pia waliachiwa huru.

Maoni:

Kuachiliwa huru kwa watu wasio na hatia ambao walikuwa wamebambikiwa kesi za ugaidi nchini Tanzania, wote Waislamu na wasiokuwa Waislamu ni hatua ya kutia moyo hususan kwa Waislamu ambao ndio wahanga wakuu wa Sheria ya ugaidi na ambao pia ni asilimia 99.9 ya watu wote waliowekwa vizuizini.

Kiuhalisia, kushindwa kwa Mkurugenzi wa Mashtaka kuwasilisha ushahidi mahakamani dhidi yao baada ya miaka mingi ya kinachoitwa “uchunguzi” inathibitisha wazi kuwa watuhumiwa hao hawana hatia yoyote na inadhihirisha hali ya kunajisiwa haki.

Kuhusiana propaganda ya vita vya ugaidi, ambayo imetengenezwa na mabepari wakoloni wamagharibi, kwa kiasi kikubwa ni mbinu ya ukoloni mamboleo ambapo wanaitumia kuingilia mifumo ya usalama ya nchi changa, kuwahonga viongozi wa nchi hizo kuua, kutesa, na kuwaweka kizuizini watu wao wasio na hatia, kuleta matabaka na mgawanyiko, kuondosha utangamano wa kijamii na kuichumi na kueneza chuki baina ya viongozi na watu wao.

Kwa upande mwingine, wakoloni wa kimagharibi kijanja hutumia matendo ya vikundi kama ISIS, ambavyo vimeleta maafa makubwa katika nchi zinazoendelea katika Afrika na sehemu nyingine duniani hususan ulimwengu wa Kiislamu. Vikundi hivi vimeleta uharibifu mkubwa kama vile vita, mauaji, ukosefu wa amani na migogoro, majanga ambapo wamagharibi wamekuwa wakitumia hali hizo kunyonya rasilimali nyingi zilizopo.

Ni jambo la kusikitisha sana kwamba suala hili (mapambano ya ugaidi) limeziburuza nchi nyingi za Afrika na nyinginezo kupoteza muda mwingi katika “kupambana na ugaidi” badala ya kutafuta njia ya kujikwamua kutoka minyororo ya ukoloni na umasikini, kinachoshangaza zaidi ni kuwa, wale wale waliotengeneza na kusambaza ugaidi ndio wanaotumia vyombo vyao vya kikoloni kama Umoja wa Mataifa (UN) kuwa wabia wao katika kupambana na ugaidi ili kuweza kudhibiti mapambano halisi.

Mnamo tarehe 28/02/22, Jumuiya ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) ilizindua Kituo cha Kupambana na Ugaidi cha Kanda (RCTC) kikiwa kama “juhudi za kuunganisha nguvu za kikanda” jijini Dar es Salaam. Uzinduzi wa kituo hiki umekuja kama juhudi za kikanda kuhusu kazi ya Jumuiya hiyo nchini Msumbiji (SADC Mission In Mozambique/SAMIM) ambayo ni kupambana na “ugaidi” na “siasa kali” kaskazini ya Msumbiji

Kama inavyotarajiwa, kituo hiki kitafanya kazi kwa maelekezo kutoka kwa mabepari Wamagharibi na tatizo halisi kamwe halitotatuliwa. Inafahamika vizuri kuwa hakukuwa na habari za ugaidi nchini Msumbiji kabla ya kugundulika kwa hifadhi kubwa ya gesi asili ambapo Total na Exxon Mobil wamewekeza mabilioni.

Maswali msingi yanayoibuka hapa ni kwa nini hadithi kuhusu ugaidi zilianza baada ya kugundulika kwa gesi na uwekezaji na sio kabla? Kwa nini ugaidi unahusishwa na kikundi kama ISIS ambacho wanasiasa wa Marekani kama aliyekuwa Raisi wa zamani bwanaTrump amekiri hadharani kuwa kikundi hicho kimetengenezwa na Marekani?

Kwa muktadha wa Tanzania, licha ya juhudi za karibuni za kuachiliwa huru baadhi ya waliowekwa kizuizini kwa tuhuma za kubambikiwa za ugaidi, bado kuna mamia ya Waislamu kama si maelfu ambao bado wapo vizuizini katika mikoa tofauti kama: Dar es Salaam, Tanga, Mwanza, Arusha, Pwani, Mtwara, Singida nk., kwa kutaja kwa uchache.

Tunataka haki itendeke kwa watu wote ambao wamewekwa kizuizini kwa uonevu, haraka iwezekanavyo wapewe dhamana au waachiwe huru.

 

Imeandikwa kwa Ajili ya Afisi Kuu ya Habari ya Hizb ut Tahrir na

Said Bitomwa

Mwanachama wa Afisi ya Habari ya Hizb ut Tahrir Tanzania

Maoni hayajaruhusiwa.