Nasaha Maalum za Eid El Fitr

بسم الله الرحمن الرحيم

Umemalizika mwezi wa baraka na tumehalalishiwa siku tukufu, siku ya Eid El Fitr ambayo Allah (SWT) ameijaalia kwa ajili ya Ummah wa Mtume (SAW) kuwa ni Sikukuu. Sisi Hizb-ut-Tahrir Tanzania tunawapa pongezi maalum Waislamu wa Tanzania na wa ulimwengu kijumla kwa munasaba wa siku hii. Tunamuomba Allah (SWT) atukubalie funga zetu, visimamo vyetu, dua zetu… hakika Yeye ni Msikivu na Mwenye kujibu dua zetu.

Enyi Waislamu:

Katika mwezi wa Ramadhani tumekushuhudieni mkijifunga katika matendo yenu kwa kipimo cha ‘halali’ na ‘haramu’ pamoja na kufanya pupa katika funga, kusimama usiku, kutoa sadaka na  kujizuiya na maovu. Tumekushuhudieni pia mukidhihirisha hisia halisi za Kiislamu… Yote hayo ni mambo ya kheri. Lakini kujifunga na amri za Allah na kujiepusha na makatazo yake si tu katika mwezi wa Ramadhani, bali ni jambo la lazima katika mwaka mzima. Na haliwi tu katika ibadat bali hujumuisha vipengee vyote vya maisha.  Basi tambueni  swala ni kama biashara, na funga ni kama bai’a, na tabia njema ni kama huduud.  Zote hizi ni ahkaam za kisheria ambazo ni wajibu kuzifuata kwa sababu zote zinatoka kwa Allah (SWT), na kujifunga nazo zote ndio kunathibitisha hasa maana ya kuwa ni waja wa Allah SWT. Allah (SWT) amesema:

﴿يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا ادْخُلُوا فِي السِّلْمِ كَافَّةً

“Enyi Mlioamini ingieni katika Uislamu wote” (TMQ Baqara: 208)

Na pia kasema Allah (SWT):

﴿وَاعْبُدْ رَبَّكَ حَتَّى يَأْتِيَكَ الْيَقِينُ

“Muabudu Mola wako mpaka yakujie mauti” (TMQ Hijr: 99)

Basi hapana budi kuuchukua Uislamu wote na kuufanya ndio wenye kutuhukumu katika maisha yetu yote hadi mauti yetu… Basi mna nini enyi Waislamu munajifunga na sharia ya Kiislamu katika mambo fulani na munaziacha katika mambo mengine, na munazitekeleza katika nyakati fulani na munaziacha katika nyakati nyengine?!

Enyi Waislamu:

Tambueni Mola wenu Mtukufu amekuhalalishieni riziki nzuri, mule na munywe katika siku yenu hii na wala musifanye israfu kwani yeye Allah (SWT) hapendi wafanyao israfu. Tumieni alivyokuruzukuni Yeye kwa ajili ya familia zenu, ingizeni furaha katika nyoyo za masikini, wajane na mayatima. Na watembeleeni jamaa zenu, wajulieni hali zao wagonjwa na walioko magerezani na fanyeni mema ili mupate kufuzu. Na tambueni kuwa sherehe ya Eid si tu kwa mwenye kuvaa nguo mpya, lakini sherehe ya Eid ni kuhofu adhabu aliyoahidi (SWT) (kwa waovu). Kwa hiyo, wasitoke nje wake zenu na mabanati zenu nusu utupu kwa kisingizio cha furaha ya Eid, kwani kufanya hivyo ni kuyadhalilisha matukufu ya Allah (SWT):

(ذَلِكَ وَمَنْ يُعَظِّمْ حُرُمَاتِ اللَّهِ فَهُوَ خَيْرٌ لَهُ عِنْدَ رَبِّهِ﴾.

“Hayo, na mwenye kutukuza matukufu ya Allah hivyo ndio bora kwake mbele ya Mola wake”. (TMQ Hajj: 30)

Enyi Waislamu:

Imemalizika Ramadhani ya 98 hali ya kuwa bado hamna Khalifah anayekutawaleni kwa mujibu wa sharia ya Allah (SWT), anayeziunganisha biladi zenu na anayebeba Uislamu kama ni ujumbe kwa walimwengu…

Imemalizika Ramadhani ya 98 bila ya Khalifah anayesimamia mambo yenu, kuhifadhi damu zenu, mali zenu, miji yenu na heshima yenu… Ndio nyinyi leo katika maeneo mbalimbali ambapo damu zenu zinamwagwa, utajiri wenu unaporwa na heshima yenu inavunjwa… Na ushahidi wa dhulma hiyo ni yale yanayowasibu Waislamu wa China ndani ya Turkistan ya Mashariki, hali katika Yemen, Palestina, Afrika ya Kati, Miyanmar, Kashmir, Afghanistan, Somalia, Mali, Libya, Al-Sham na kwengineko… Hivyo,  yote haya hayakupelekeeni kufikiri maana ya hadithi ya Mtume (SAW):

«إِنَّمَا الْإِمَامُ جُنَّةٌ يُقَاتَلُ مِنْ وَرَائِهِ وَيُتَّقَى بِهِ»، رواه مسلم.

Hakika ya Imamu (Khalifah) ni ngao, (Waislamu) hupigana nyuma yake na hujikinga kwake” (Muslim)

Mwisho, sisi Hizb-ut-Tahrir Tanzania tunakutakieni baraka za Eid hii tukufu. Tunatoa mwito kwa watu wote kutonyamazia dhulma inayoletwa na mfumo wa ubepari, na pia wafanye utafiti kwa uadilifu kuhusu sharia za Kiislamu na masuluhisho yake (kwa matatizo ya mwanadamu). Aidha, maalumu tunawalingania Waislamu katika nchi za Kiislamu kubeba da’wa ya Uislamu ili kurejesha tena maisha ya Kiislamu kwa kusimamisha Khilafah kwa njia ya Utume.

Hizb-ut-Tahrir Tanzania

Tarehe 01 Shawal 1440 Hijri

Maoni hayajaruhusiwa.