Hizb ut Tahrir Tanzania inatoa Mwito Kuachiwa Huru Mahabusu wote 12 Waliokamatwa Kwa Mara ya Pili
بسم الله الرحمن الرحيم
Taarifa kwa Vyombo vya Habari
Hizb ut Tahrir / Tanzania inalaani kwa nguvu zote kitendo cha kukamatwa tena mara ya pili kwa wanaodaiwa kuwa watuhumiwa wa ugaidi ambao waliachiwa huru tarehe 4 Machi 2025 baada ya kushikiliwa kwa miaka kumi.
Watuhumiwa wenyewe ni wafuatao:
1. Ali Mohammed Ulatule (70)
2. Khamisi Mohammed Ulatule (61)
3. Nassoro Suleiman Ulatule
4. Rajab Ali Mohammed Ulatule
5. Na Ramadhani Khamisi Mohammed Ulatule
6. Saidi Abdallah Chambeta
7. Fadhili Shaabani Lukwembe
8. Mnemo Qassim Mwatumbo
9. Abdallah Bushiri Kalukula
10. Khamisi Ally Masamba
11. Omari Abdallah Makota
12. Mohammed Hassan Ungando
Watuhumiwa wote hao waliotajwa waliachiwa huru wiki iliyopita baada ya Afisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) kutangaza kwamba haina dhamira ya kuendelea na shauri lao, lakini kwa ukatili bila ya haya vyombo vya dola vimewatia tena nguvuni na kuwaweka mahabusu katika mwezi huu mtukufu wa Ramadhani.
Ni jambo la kuhuzunisha sana kwamba vyombo vya dola vimewaweka tena watu hao mahabusu kwa mara ya pili bila ya kujali misingi ya utu, kwa kuwa mahabusu hao walikwishawekwa mahabusu kabla kwa muda mrefu bila ya hatia chini ya kisingizio cha dhulma cha “Uchunguzi Unaendelea”, ilhali miongoni mwao wakiwa na umri mkubwa, baadhi kutoka familia moja (Namb 1-5) ambao awali walikuwa watu saba, kwa masikitiko makubwa wawili wamefariki wakiwa ndani ya mahabusu. Zaidi ya yote hayo hakuna malipo yoyote ya fidia watakayopewa.
Hizb ut Tahrir Tanzania imekuwa ikisema mara nyingi kwamba Sheria ya Kupambana na Ugaidi ni sheria ya kigeni ya kikoloni yenye misingi ya dhulma ikigubikwa na mengi ya kutia shaka katika miamala yake kwa kesi zinazoitwa za ugaidi kwa Waislamu wa Tanzania na penginepo. Miongoni mwa ya maswala msingi katika uendeshaji wa kesi hizo kesi ni kwanini ushahidi wa kesi hizo hauwasilishwi mbele ya mahkama? Kwanini watuhumiwa hawapewi haki ipasavyo ya kesi zao kusikilizwa kwa muda muwafaka? Kwanini watuhumiwa hawapewi dhamana? Kwa nini wakati mwengine watuhumiwa hukamatwa tena mara ya pili baada ya kuachiwa huru? nk.
Jibu pekee linalodhihirika kwa maswala hayo ni uwepo wa ajenda ya kidhulma kwa kisingizio cha kupambana na ugaidi.
𝐇𝐢𝐳𝐛 𝐮𝐭 𝐓𝐚𝐡𝐫𝐢𝐫 𝐓𝐚𝐧𝐳𝐚𝐧𝐢𝐚 inatoa mwito kwa Waislamu na wapenda haki wote kupaza sauti zao dhidi ya kitendo hiki cha kunajisi haki, pia tunazitaka taasisi zote za kusimamia haki nchni Tanzania kushikamana na maamuzi ya Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) kwa kuwaachia huru mara moja watuhumiwa wote 12.
Masoud Msellem
Maoni hayajaruhusiwa.